ELECTIONS COMMITTEE
                       TAARIFA KWA VYOMBO YA HABARI
06 MACHI 2012
UFAFANUZI KUHUSU MAJUKUMU, WAJIBU NA MAMLAKA YA KAMATI YA UCHAGUZI NA
 MAELEZO YA KINA KUHUSU MAAMUZI YA KAMATI ZA UCHAGUZI ZA TFF KUHUSU MAOMBI 
YA NDG. MICHAEL RICHARD WAMBURA KUGOMBEA UONGOZI KWENYE UCHAGUZI WA 
TFF 2008, UCHAGUZI WA KLABU YA SIMBA 2010 NA FAM 2011.
1.                   USIMAMIZI WA CHAGUZI ZA WANACHAMA WA TFF
            Muundo wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) umeelezwa wazi kwenye Katiba ya TFF Ibara ya 18. Kamati ya Uchaguzi ya TFF ni moja kati ya vyombo sita vilivyoainishwa
 katika Muundo wa TFF. Majukumu, wajibu na mamlaka ya vyombo vya TFF 
yameainishwa katika Katiba ya TFF na Kanuni zilizotungwa na kuidhinishwa
 na Kamati ya Utendaji ya TFF kwa kuzingatia Ibara ya 34 ya Katiba hiyo.
            Majukumu,
 wajibu na mamlaka ya Kamati ya Uchaguzi ya TFF yameainishwa kwenye 
Katiba ya TFF Ibara ya 49 na kwenye Kanuni za Uchaguzi za TFF na Kanuni 
za Uchaguzi za wanachama wa TFF. Mbali na majukumu na wajibu wa 
kusimamia uchaguzi wa TFF na chaguzi za wanachama wake na kuishauri 
Kamati ya Utendaji ya TFF kuhusu Kanuni za Uchaguzi, Kamati ya Uchaguzi 
ya TFF inao wajibu wa kulinda Katiba na Kanuni za uchaguzi za TFF na 
Katiba ya FIFA na Katiba za wanachama wa TFF kama ilivyotamkwa kwenye 
Kanuni za Uchaguzi za TFF Ibara ya 6 na Kanuni za Uchaguzi za wanachama 
wa TFF Ibara ya 26.
 Uchaguzi Mkuu wa TFF hufanyika kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi wa TFF.
 Chaguzi za wanachama wa TFF na wanachama wao hufanyika kwa mujibu wa 
Kanuni za uchaguzi za wanachama wa TFF na si vinginevyo. Kanuni hizi 
zimeainisha taratibu mbalimbali ambazo lazima zizingatiwe kikamilifu, 
ikiwa ni pamoja na utaratibu wa ukataji rufaa katika ngazi mbalimbali za
 uchaguzi. Vyombo na Kamati zote za  TFF,
 Wanachama wote wa TFF na wanachama wao, na wadau wote wa soka wanao 
wajibu wa kuheshimu Kanuni mbali mbali za TFF ambazo ni pamoja na Kanuni
 za Uchaguzi.
2.                   MAAMUZI KUHUSU MAOMBI YA UONGOZI YA NDG. MICHAEL WAMBURA 
Kwa
 muda mrefu pamekuwepo na taarifa mbalimbali kupitia vyombo vya habari 
zenye lengo la kuwafanya wadau na wapenzi wa soka na umma wa watanzania 
kwa ujumla kuaminishwa kuwa Ndg. Michael Wambura huonewa na vyombo vya 
TFF vinavyosimamia uchaguzi kila anapoomba nafasi za uongozi katika TFF.
 Baadhi ya vyombo vya habari na baadhi ya wapenzi wa soka wamesikika 
wakisema kwamba kuenguliwa kwa Ndg. Michael Wambura kugombea uomgozi ni 
kutokana na kuogopwa na viongozi wa TFF. Kamati ya Uchaguzi ya TFF 
inapenda kufafanua kwa kina maamuzi yote yaliyofanyika kuhusu maombi 
yote ya uongozi ya Ndg. Michael Wambura na kuweka wazi vielelezo 
vilivyotumika kufikia maamuzi hayo ili umma wa watanzania wafahamu 
kinagaubaga ukweli kuhusu maamuzi hayo:
            UCHAGUZI MKUU WA TFF 2008
            Kamati
 ya Uchaguzi ya TFF ilimwengua Ndg. Michael Wambura kugombea nafasi ya 
Makamu wa kwanza wa Rais wa TFF kwa kutokidhi matakwa ya uadilifu kwa 
mujibu wa Kanuni za Uchaguzi na Katiba ya TFF. Ndg. Michael Wambura 
hakuridhika na uamuzi huo na alikata rufaa kwenye Kamati ya Rufaa ya 
TFF. Hata hivyo baada ya Kamati ya Rufaa kupitia nyaraka mbali mbali 
zilizowasilishwa kwenye Kamati hiyo ikiwa ni pamoja na ripoti ya ukaguzi
 wa maheabu ya TFF/FAT kwa mwaka 2002, 2003 na 2004 rufaa yake 
ilishindwa baada ya Kamati ya Rufaa kuridhika na kuweka bayana kuwa 
mwomba rufaa, Michael Richard Wambura aliipa Zabuni kampuni yake iitwayo
 Min Investments & Commercial Services Co. wakati akiwa Katibu Mkuu wa FAT/TFF na hivyo kushindwa kukudhi kigezo cha uadilifu.
 Katika kufikia maamuzi yake, Kamati ya rufaa pia ilibaini kuwa Ndg. 
Michael Richard Wambura alionyesha kuwa alikuwa amechana na umiliki wa 
kampuni hiyo kuanzia tarehe 12 Novemba 2003 kwa mabadiliko 
yaliyotekelezwa tarehe 28 Februari 2007 kwa malipo ya Shs. 34,500/= ya “exchequer receipt No. 28173444’.
 Hata hivyo, Kamati ya Rufaa iliridhika kuwa utekelezaji wa mabadiliko 
ya umiliki wa kampuni hiyo ulichukua takribani miezi arobaini (40). 
Baada ya majadiliano ambayo yalikuwa yamekitwa (pegged) kwenye uadilifu (integrity), Kamati ya Rufaa iliridhika kuwa taswira inayojitokeza kwenye muktadha imegubikwa na wingu jeusi la mashaka kuhusu “integrity” ya Muomba Rufaa (Ndg. Michael Richard Wambura).
            Uthibitisho kwamba mmilki wa Kampuni ya Min Investments & Commercial Services Co
 ni Ndg. Michael Richard Wambura ulitolewa na Msajili wa Makampuni 
(Business Registration and Licensing Agency-BRELA) kwa barua yenye 
Kumbukumbu Na. MITM/RBN/93017 ya tarehe 16 Agosti 2006. Kampuni hiyo 
ilisajiliwa tarehe 17 Julai 1992.
            Kamati ya Uchaguzi ya TFF inatoa sehemu ndogo tu ya ubadhirifu uliokuwa unafanywa kwa kutumia Kampuni hiyo (Min Investments & Commercial Services Co)
 ya Michael Wambura kinyume na utaratibu wa utoaji tenda wa FAT/TFF na 
malipo aliyojilipa bila maelezo yoyote kama ilivyoainishwa kwenye Ripoti
 ya Ukaguzi wa Mahesabu iliyowasilishwa na wakaguzi tarehe 19 Septemba 
2005 na Ripoti maalumu ya ukaguzi iliyowasilishwa Novemba 2006, kama 
ifuatavyo:
(i)       Tarehe
 28 Julai 2004 Michael Wambura akiwa Katibu Mkuu wa TFF alilipwa Dola za
 Kimarekani 16,548.00 (US$ 16,548 sawa na Tshs. 17,170,040 wakati huo) 
kwa ununuzi wa samani (furniture) za Hosteli ya TFF. Pesa hizo 
zilizoombwa kulipwa kwa Michael Wambura zimeonyeshwa kwenye fomu ya 
malipo ya TFF ya tarehe 28 Julai 2004. Pesa hizo zilipokelewa na Kampuni
 ya Min Investments & Commercial Services Co
 na kuthibitisha kupokelewa na kampuni hiyo kwa risiti Na. 020 ya tarehe
 21 Julai 2004 ya kampuni hiyo, ingawa hapakuwa na maombi ya manunuzi 
(order) iliyokuwa imefanywa na TFF kwa kampuni hiyo.  
(ii)     Baada
 ya kujilipa pesa zilizotajwa hapo juu, kesho yake tarehe 29 Julai 2004 
Ndg. Michael Wambura akiwa Katibu Mkuu wa TFF alijilipa Dola za 
kimarekani 25,000.00 (US$ 25,000.00 sawa na Tshs. 25,937,500 wakati 
huo), kama ilivyoonyeshwa kwenye vocha ya malipo ya TFF Na. 5324 ya 
tarehe tajwa hapo juu, ikionyesha kuwa ni kwa ajili ya malipo ya samani 
za Hosteli (US$ 15,000.00) na malipo ya awali ya Gari (US$ 10,000.00). 
Ndg. Michael Wambura alithibitisha kupokea malipo hayo. Ripoti ya 
Ukaguzi inabainisha wazi kuwa vifaa vichache vilivyonuliwa kwa hosteli 
ya TFF thamani yake haikuainishwa na hapakuwa na gari lililolipiwa 
malipo ya awali katika vitabu vya mahesabu ya TFF.
(iii)    Katika
 kipindi cha mwaka 2002 Ndg. Michael Wambura akiwa Katibu Mkuu wa FAT 
alijikopesha jumla ya Tshs. 36,850,750 bila idhini ya Kamati ya 
Utendaji.
(iv)    Tarehe 20 Mei 2002 Ndg. Michael Wambura akiwa Katibu Mkuu wa FAT alijilipa Tshs. 12,147,837 ambazo hazina maelezo yoyote.
(v)     Imebainishwa
 wazi kuwa FAT/TFF ilikuwa mfilisi katika kipindi cha 2002-2004 (Nukuu: 
“The Association was actually insolvent during the period.”)
            Kamati
 inaweka wazi tena kwamba maamuzi yaliyofikiwa na Kamati ya Rufaa ya 
kumuengua Michael Wambura kwenye uchaguzi Mkuu wa TFF yanaweza tu 
kubadilishwa na Mahakama ya usuluhishi wa masuala ya michezo (CAS) 
endapo Michael Wambura atakata rufaa CAS kupinga maamuzi hayo na 
kushinda rufaa, na si vinginevyo.
            MAAMUZI YA MKUTANO MKUU WA TFF 2007
            Mkutano Mkuu wa TFF ambacho ndicho chombo cha juu kabisa cha TFF (Supreme Authority of TFF)
 katika kikao chake mwaka 2007 kilipitia ripoti za ukaguzi wa mahesabu 
ya FAT/TFF kwa kipindi cha mwaka 2002 hadi 2004 na baada ya kujiridhisha
 kuhusu ubadhirifu uliofanywa na Ndg. Michael Wambura, Mkutano Muu wa 
TFF uliamua kwamba Ndg.
 Michael Wambura afikishwe kwenye vyombo vya dola kwa ubadhirifu wa 
fedha za FAT/TFF alioufanya kama ilivyoainishwa kwenye ripoti za ukaguzi
 wa Mahesabu. Sekretarieti ya TFF mwaka 2007 ikitekeleza maagizo ya 
Mkutano Mkuu wa TFF na suala hilo lilpelekwa Jeshi la Polisi. Jeshi la Polisi ilithibitisha maombi ya TFF kwa barua  yake ya tarehe 18 Januari 2008 na kumfungulia jalada  Ndg Michael Wambura kwa kosa la wizi  akiwa Mtumishi. Kamati ya Uchaguzi ya TFF inaheshimu maamuzi ya Mkutano Mkuu wa TFF na hadi sasa haijataarifiwa kwa maandishi na chombo chochote kama suala hilo limefikia ukomo wa aina yoyote. 
            UCHAGUZI WA KLABU YA SIMBA MWAKA  2010
            Ndg.
 Michael Richard Wambura aliomba kugombea nafasi ya Mwenyekiti wa Klabu 
ya Simba. Hata hivyo alikatiwa rufaa na Ndg. Daniel T. Kamna  kwa
 kutotimiza matakwa ya Ibara ya 9 ya Kanuni za Uchaguzi za wanachama wa 
TFF kama ilivyoamuliwa na Kamati ya Uchaguzi ya TFF na pia Kamati ya 
Rufaa ya TFF mwaka 2008 wakati alipoomba kugombea nafasi ya Makamu wa 
kwanza wa Rais wa TFF. Kamati ilikubaliana na maamuzi yaliyotolewa na 
Kamati ya Uchaguzi na Kamati ya Rufaa ya TFF mwaka 2008 kwamba Bw. 
Michael R. Wambura  si mwadilifu  kama
 ilivyonyeshwa kwenye aya ya 2.1 na 2.2 hapo juu na hivyo hakukidhi 
matakwa ya Ibara ya 29(7) ya Katiba ya TFF na Ibara ya 9 ya Kanuni za 
Uchaguzi za wanachama wa TFF.  Kamati ilimuondoa kugombea nafasi ya Mwenyekiti wa Simba SC.
            Baada
 ya maamuzi hayo ya Kamati, Ndg. Michael Richard Wambura alikwenda 
Mahakamani na akafungua kesi kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es salaam
 dhidi ya Mwenyekiti wa Klabu ya Simba kuzuia uchaguzi wa klabu ya Simba
 usifanyike. Kwa kufanya hivyo alivunja Katiba ya Klabu ya Simba na 
kukiuka Katiba ya TFF Ibara ya 12(2) (e) na Katiba ya FIFA Ibara ya 
64(2). Klabu ya Simba ilichukua hatua za kikatiba, na katika kikao chake
 cha 5/5/2010, ilimsimamisha uanachama Ndg. Wambura kwa kukiuka katiba 
ya klabu hiyo. Klabu ya Simba iliitaarifu TFF uamuzi huo kwa barua yenye
 Kumbukumbu Na. SSC/MMKT/162/Vol.40/10 ya tarehe 06 Mei 2010 
iliyoambatanishwa na Muhtasari wa kikao cha Kamati ya Utendaji 
kilichofanya uamuzi huo. Uamuzi wa kumrudishia uanachama unafanywa na 
Mkutano Mkuu wa Klabu ya Simba. TFF haijapokea taarifa yoyote kutoka 
Klabu ya Simba kwamba Mkutano Mkuu wa Klabu hiyo ulikwisha msamehe. Kwa 
hali hiyo taarifa ya kusimamishwa kwake iliyotumwa TFF mwezi Mei 2010 
itaendelea kuzingatiwa hadi hapo Klabu ya Simba itakapo ijulisha TFF 
mabadiliko ya maamuzi hayo.
3.                   MAAMUZI KUHUSU UCHAGUZI WA FAM
            Kamati
 ya Uchaguzi ya TFF ilimuondoa Ndg. Michael Wambura kugombea nafasi ya 
Mwenyekiti wa FAM kwa kuwa alifungua kesi kwenye Mahakama ya Hakimu 
Mkazi Kisutu, Dar es salaam dhidi ya Mwenyekiti wa Klabu ya Simba akiwa 
ni mwanachama wa Klabu ya Simba kuzuia uchaguzi wa klabu ya Simba 
usifanyike, jambo ambalo ni uvunjaji wa Katiba ya Klabu ya Simba, 
ukiukwaji wa Katiba ya FAM, TFF na FIFA. 
            Pia, Kamati ya Uchaguzi ya TFF iliweka wazi kama
 ilivyobainisha kwenye uchaguzi wa Klabu ya Simba kwamba suala la 
uadilifu wa Ndg. Wambura lilishafanyiwa maamuzi na Kamati ya Rufaa ya 
TFF mwaka 2008 kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi Mkuu wa TFF. Kwa mujibu 
wa Kanuni za Uchaguzi huo na Katiba ya TFF Mamlaka pekee inayoweza 
kutengua uamuzi huo ni Mahakama ya Usuluhishi wa masuala ya Michezo 
(CAS) iliyo na makao yake Lausanne, Switzerland.
            Baada
 ya uamuzi huo, Kamati ya Uchaguzi ya TFF imeshuhudia baadhi ya vyombo 
vya TFF vikishughulikia masuala ya uchaguzi kinyume na matakwa ya Katiba
 ya TFF na Kanuni za Uchaguzi, kama ifuatavyo:
(i)       Katika
 hali isiyozingatia Kanuni za Uchaguzi za wanachama wa TFF, Kamati ya 
Nidhamu ilipokea malalamiko ya Ndg. Michael Wambura yaliyoitwa ‘rufaa’. 
Kwa kuwa hakuna utaratibu wa masuala ya uchaguzi kukatiwa rufaa kwenye 
Kamati za nidhamu katika ngazi zote za uchaguzi na hivyo pia kutokuwepo 
ada ya ‘rufaa’ za aina hiyo, mlalamikaji alilazimisha kupokelewa ada ya 
Tshs 300,000/= ambayo ni ada inayotumika kwa rufaa za Ligi Kuu ya Vodacom ambayo imeainishwa katika Ibara ya 17 ya kanuni za mashindano hayo. Ada
 hiyo iliwekwa (deposited) kwenye Akaunti ya TFF bila ridhaa ya TFF. 
Pamoja na mapungufu hayo “rufaa’ hiyo ilisikilizwa na Kamati ya Nidhamu 
na kutolewa maamuzi. Mlalamikaji hakuridhika na maamuzi ya Kamati hiyo 
na aliamua kukata ‘rufaa’ katika Kamati ya Rufaa ya TFF. 
(ii)     Kamati
 ya Rufaa ya TFF ilipokea na kusikiliza ‘rufaa’ ya Ndg. Michael Richard 
Wambura, kinyume na matakwa ya Kanuni za Uchaguzi za wanachama wa TFF. 
Kwa kuwa kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi za wanachama wa TFF hakuna 
rufaa inayokatwa kwenye Kamati hiyo, hivyo kutokuwapo ada yoyote kwa 
“rufaa” ya aina hiyo, ili kutimiza azma ya kusikiliza ‘rufaa’ hiyo, 
palifanyika juhudi za kulazimisha kupokelewa ‘ada’ ya Shilingi 500,000/=
 ambayo ni ada ya rufaa za mashindano ya Ligi Kuu ya Vodacom ambayo 
imeainishwa pia katika Ibara ya 17 ya kanuni za mashindano ya Ligi Kuu ya Vodacom. Hata hivyo, ada hiyo ambayo si halali, haikupokelwa na Sekretarieti ya TFF  baada ya kushindikana kuainisha ada ya mashindano ya Ligi Kuu ya Vodacom na masuala ya Uchaguzi.  Bila kuzingatia Kanuni za Uchaguzi za wanachama wa TFF na Katiba ya TFF Ibara ya 47(4) inayotamka na kuikataza Kamati ya Rufaa  kusikiliza rufaa kwa mambo yaliyowekewa ukomo na Kanuni husika; Ibara hiyo inatamka; ‘The
 Appeal Committee shall be responsible for hearing appeals against 
decisions from the Disciplinary Committee that are not declared final by
 relevant regulations as well as decision passed by the players’ Status 
Committee concerning the eligibility of players for the teams’, 
Kamati hiyo ilisikiliza malalamiko ya Ndg. Michael Richard Wambura na 
kutoa uamuzi bila kuzingatia Kanuni za Uchaguzi za wanachama wa TFF 
ambazo ni ‘relevant regulations’ na Ibara ya 12(4) ya Kanuni hizo 
kutamka wazi kuwa;  ‘The decisions of the TFF Elections Committee are final and conclusive and shall not be monitored by any other body’.
(iii)    Kamati
 ya Uchaguzi ya TFF inatamuka wazi kuwa utaratibu mzima uliotumika 
kupokea rufaa hiyo toka Kamati ya Nidhamu hadi ya Kamati ya Rufaa 
haukufanyika kwa mujibu wa taratibu za ukataji rufaa zilizoainishwa 
kwenye Kanuni za Uchaguzi za wanachama wa TFF.  Ukataji
 rufaa huo uliongozwa zaidi na hila kuliko dhamira ya kuheshimu taratibu
 zilizowekwa. Mbali na kutumia kanuni za Ligi kuu ya Vodacom kusikiliza 
‘rufaa’ hizo, uthibitisho mwingine wa hila na ujanjaujanja ni pale 
mlalamikaji alipokwenda kuweka kwenye akaunti ya TFF ada ya rufaa ya 
mashindano ya Ligi Kuu ambayo haitambuliki kwa mujibu wa Kanuni za 
Uchaguzi na kutumia vyombo vya habari kutangaza kitendo hicho, lakini 
baada ya kutolewa maamuzi na Kamati ya Rufaa alienda kimya kimya TFF 
kuchukua ada hiyo ambayo ni ya rufaa kwa mashindano ya Ligi kuu.
(iv)    Kamati
 ya Uchaguzi ya TFF, kwa mamlaka yaliyo kasimiwa kwake na Katiba ya TFF 
Ibara ya 49(1) , Kanuni za Uchaguzi za TFF Ibara ya 6, Kanuni za 
Uchaguzi za wanachama wa TFF Ibara ya 8(2), 10(6), 12(4) na 26(2), na 
pia kwa mamlaka yaliyoainishwa katika Katiba za wanachama wa TFF kuhusu 
uchaguzi, katika kikao chake kilichofanyika 03 Desemba 2011 iliamua na 
inatamka wazi kuwa maamuzi yaliyofanywa na Kamati ya Rufaa ni BATILI kwa
 kuwa hayakuzingatia Kanuni za Uchaguzi za wanachama wa TFF. Kamati ya 
Uchaguzi ya TFF inaziagiza Kamati zote za Uchaguzi za wanachama wa TFF 
na wanachama wao kuendelea kuzingatia Kanuni za Uchaguzi katika utendaji
 wa kazi zao za kuendesha na kusimamia chaguzi zote za vyama vya mpira 
wa miguu nchini, ikiwa ni pamoja na kutozingatia maamuzi yoyote ya 
uchaguzi yatakayofanyika kinyume na Kanuni za Uchaguzi.
4.                   TAARIFA ZA UDANGANYIFU KUTOKA KWA BAADHI YA WAGOMBEA UONGOZI KWENYE VYAMA WANACHAMA WA TFF.
            Kamati
 ya Uchaguzi inapenda kuwakumbusha wadau wote wa soka wenye nia ya 
kugombea uongozi TFF na vyama wanachama wa TFF kuwa kwa mujibu wa Kanuni
 za Uchaguzi za TFF ibara ya 25(8) na Kanuni za Uchaguzi za wanachama wa
 TFF Ibara ya 26(8)  ni makosa kuwasilisha taarifa za udanganyifu kwenye Kamati ya Uchaguzi. Kanuni hizo zinatamka kuwa; During
 the election process any person or member who contravenes this code or 
provides false particulars or qualification, may be penalized to a fine 
not exceeding five hundred thousand shillings or be barred to 
participate in the election process for 2 years or for both a fine and 
such barring, provided that the General Secretary lodges a complaint to 
the TFF judicial organ for disciplinary action.
            Kamati
 imebaini kuwa baadhi ya wagombea walifanya udanganyifu kuhusu vyeti 
halisi walivyowasilisha kwenye uchaguzi wa FAM na pia baadhi ya waombaji
 uongozi katika uchaguzi wa klabu ya Villa. Kwa mfano mwombaji aliyeomba
 kugombea nafasi ya Mwenyekiti wa Klabu ya Villa cheti chake cha Elimu 
ya Msingi alichowasilisha kwenye Kamati ya Uchaguzi kina utata. Vyote 
hivyo viko katika hatua za uhakiki kwenye mamlaka husika, uhakiki 
utakapokamilika Kamati itachukua hatua kwa mujibu wa Kanuni tajwa hapo 
juu.
            Kamati
 imebaini na kujiridhisha kuwa Ndg. Michael Wambura alitoa taarifa 
zinazokinzana kwenye Kamati ya Uchaguzi kuhusu umri wake. Katika 
Uchaguzi wa Klabu ya Simba mwaka 2010, aliwasilisha taarifa kwamba 
amezaliwa mwaka 1967 lakini katika uchaguzi wa Chama cha Mpira wa Miguu 
Mkoa wa Mara aliwasilisha taarifa kwamba alizaliwa mwaka 1965. Taarifa 
za umri zinazokinzana za mwombaji uongozi zinashiria mashaka ya umakini 
na uadilifu wa mgombea hasa ikizingatiwa kuwa nafasi ya uongozi ya 
mwenyekiti kwa vyama wanachama wa TFF na  Rais wa TFF zina ukomo wa wa umri. Kamati itachukua hatua zilizoainishwa kwenye Kanuni za Uchaguzi tajwa hapo juu.
5.                   KAULI ZENYE LENGO LA KUVURUGA CHAGUZI ZA WANACHAMA WA TFF.
            Katika siku za karibuni Kamati ya Uchaguzi ya TFF imeshuhudia kauli amabazo si za kiwanamichezo zenye lengo la kuleta vurugu katika michakato ya Uchaguzi. Kwa mfano
 kauli za kuwahamasisha wadau wa soka kwenda mahakamani kwa masuala ya 
michezo, hususan, kupinga michakato ya uchaguzi ni uvunjaji wa Kanuni za
 Uchaguzi na Katiba ya TFF na FIFA. Kamati inawataka wadau wote wa soka 
kuheshimu na kuzingatia Kanuni na taratibu za uchaguzi na Katiba ya TFF,
 vinginevyo Kamati haitasita kuchukua hatua stahiki kwa mujibu wa Kanuni
 za Uchaguzi.
Deogratias J. Lyatto
MWENYEKITI
KAMATI YA UCHAGUZI
SHIRIKISHO LA MPIRA WA MIGUU TANZANIA
chanzo na Shaffi Dauda
chanzo na Shaffi Dauda
No comments:
Post a Comment