Ryan Giggs, alikuwa na usiku 
wa aina yake baada ya kufanikiwa kujiwekea historia ya kuwa mchezaji 
mwenye umri mkubwa zaidi kuwahi kufunga katika michuano ya klabu bingwa 
Ulaya na kuisaidia klabu yake ya Manchester United kufanikiwa kupata 
sare ya bao 1-1 dhidi ya Benfica ya Ureno.
Katika pambano hilo ambalo lilikuwa wazi
 kwa timu zote huku yeyote kati ya timu hizo mbili akionekana angeweza 
kuibuka na ushindi ndani ya dakika tisini za mchezo, wenyeji 
walitangulia kufunga kupitia kwa Oscar Cardozo kunako dakika ya 24 ya 
mchezo.
Alifunga bao hilo baada ya kutumia 
makosa ya mabeki wa United, ambapo aliachia shuti kali la umbali wa 
takriban mita 18 hivi lililomshinda mlinda mlango wa United na baada ya 
hapo wenyeji wakaonekana kama wangeongeza bao wakati wowote.
Hata hivyo, dakika chache kabla ya 
mapumziko, Ryan Giggs alipokea pasi safi toka wingi ya kulia mwa uwanja 
kabla ya kukokota mpira huku akiwadhibiti mabeki kadhaa wa Benfica na 
kisha kuachia mkwaju safi na kuandika bao la kusawazisha, na matokeo 
hayo yakasimama hivyo hadi wakati wa mapumziko.
Kipindi cha pili kilishuhudia timu zote 
zikifanya mabadiliko kadhaa sanjari na kucheza kandanda safi lakini 
zaidi ya kosakosa kadhaa kwa kila upande, hakuna timu iliyoweza kuliona 
lango la mwenzie na hivyo hadi mwisho wa mchezo Benfica 1-1 United.

Ryan Giggs awa mchezaji mkongwe zaidi kufunga katika ligi ya mabingwa Ulaya
Bao la Giggs linamfanya aweke rekodi ya 
kuwa mchezaji mkongwe zaidi kufunga katika michuano hiyo akiwa na umri 
wa miaka 37 na siku 289, ambapo pia anampita mkongwe Raul Gonzalez kwa 
kuwa mchezaji aliyefunga katika misimu mingi zaidi ya michuano hiyo, 
akiwa amefikisha misimu 16 hivi sasa.
Wakati United wakiambulia sare ya 
ugenini, jirani zao Manchester City nao walijikuta wakiambulia sare ya 
nyumbani dhidi ya Napoli kwenye mechi ambayo wageni Napoli walitangulia 
kufunga kupitia kwa Edinson Cavani lakini wenyeji wakajitutumua na 
kusawazisha kupitia kwa Aleksander Kolarov dakika chache baadae.
Kule nchini Uholanzi, Ajax walibanwa 
vilivyo na waliokuwa wageni wao Lyon ya kutokea nchini Ufaransa na 
kuambulia sare ya bila kufungana lakini miamba ya Hispania Real Madrid 
wakianza michuano hiyo vyema baada ya kuchomoza na ushindi wa bao 1-0 wa
 ugenini kwenye uwanja wa Dinamo Zagreb, bao pekee la mchezo huo 
likiwekwa kimiani na Angel Di Maria.
Mechi zingine za usiku huu zimeshuhudia 
FC Basle wakiibuka na ushindi wa bao 2-1 dhidi ya SC Otelul Galati, huku
 Inter Milan wakianza vibaya baada ya kukubali kichapo cha nyumbani cha 
bao 1-0 toka kwa Trabzonspor.
Nao wafaransa Lille wakiwa nyumbani 
wakaambulia sare ya bao 2-2 dhidi ya CSKA Moscow Ilhali Villarreal 
wakiwaruhusu wageni wao Bayern Munich kuwaadhiri nyumbani kwa kichapo 
cha bao 2-0
No comments:
Post a Comment