Sep 20, 2011

Giggs aweka rekodi United wakianza kwa sare

Ryan Giggs, alikuwa na usiku wa aina yake baada ya kufanikiwa kujiwekea historia ya kuwa mchezaji mwenye umri mkubwa zaidi kuwahi kufunga katika michuano ya klabu bingwa Ulaya na kuisaidia klabu yake ya Manchester United kufanikiwa kupata sare ya bao 1-1 dhidi ya Benfica ya Ureno.
Katika pambano hilo ambalo lilikuwa wazi kwa timu zote huku yeyote kati ya timu hizo mbili akionekana angeweza kuibuka na ushindi ndani ya dakika tisini za mchezo, wenyeji walitangulia kufunga kupitia kwa Oscar Cardozo kunako dakika ya 24 ya mchezo.
Alifunga bao hilo baada ya kutumia makosa ya mabeki wa United, ambapo aliachia shuti kali la umbali wa takriban mita 18 hivi lililomshinda mlinda mlango wa United na baada ya hapo wenyeji wakaonekana kama wangeongeza bao wakati wowote.
Hata hivyo, dakika chache kabla ya mapumziko, Ryan Giggs alipokea pasi safi toka wingi ya kulia mwa uwanja kabla ya kukokota mpira huku akiwadhibiti mabeki kadhaa wa Benfica na kisha kuachia mkwaju safi na kuandika bao la kusawazisha, na matokeo hayo yakasimama hivyo hadi wakati wa mapumziko.
Kipindi cha pili kilishuhudia timu zote zikifanya mabadiliko kadhaa sanjari na kucheza kandanda safi lakini zaidi ya kosakosa kadhaa kwa kila upande, hakuna timu iliyoweza kuliona lango la mwenzie na hivyo hadi mwisho wa mchezo Benfica 1-1 United.
Ryan Giggs awa mchezaji mkongwe zaidi kufunga katika ligi ya mabingwa Ulaya
Bao la Giggs linamfanya aweke rekodi ya kuwa mchezaji mkongwe zaidi kufunga katika michuano hiyo akiwa na umri wa miaka 37 na siku 289, ambapo pia anampita mkongwe Raul Gonzalez kwa kuwa mchezaji aliyefunga katika misimu mingi zaidi ya michuano hiyo, akiwa amefikisha misimu 16 hivi sasa.
Wakati United wakiambulia sare ya ugenini, jirani zao Manchester City nao walijikuta wakiambulia sare ya nyumbani dhidi ya Napoli kwenye mechi ambayo wageni Napoli walitangulia kufunga kupitia kwa Edinson Cavani lakini wenyeji wakajitutumua na kusawazisha kupitia kwa Aleksander Kolarov dakika chache baadae.
Kule nchini Uholanzi, Ajax walibanwa vilivyo na waliokuwa wageni wao Lyon ya kutokea nchini Ufaransa na kuambulia sare ya bila kufungana lakini miamba ya Hispania Real Madrid wakianza michuano hiyo vyema baada ya kuchomoza na ushindi wa bao 1-0 wa ugenini kwenye uwanja wa Dinamo Zagreb, bao pekee la mchezo huo likiwekwa kimiani na Angel Di Maria.
Mechi zingine za usiku huu zimeshuhudia FC Basle wakiibuka na ushindi wa bao 2-1 dhidi ya SC Otelul Galati, huku Inter Milan wakianza vibaya baada ya kukubali kichapo cha nyumbani cha bao 1-0 toka kwa Trabzonspor.
Nao wafaransa Lille wakiwa nyumbani wakaambulia sare ya bao 2-2 dhidi ya CSKA Moscow Ilhali Villarreal wakiwaruhusu wageni wao Bayern Munich kuwaadhiri nyumbani kwa kichapo cha bao 2-0

No comments: